Monday, May 9, 2016

KALENDA YA UFUGAJI NYUKI TANZANIA.

KALENDA YA UFUGAJI NYUKI TANZANIA.


Kalenda ya Ufugaji Nyuki ni mwongozo kwa Mfugaji Nyuki kujua majira katika eneo analofugia ili kuweza kupanga ratiba ya kazi za kusimamia makundi ya Nyuki.Katika nchi za kitropiki kuna vipindi vya kiangazi na vipindi vya mvua sio kama nchi za baridi ambapo kuna majira ya vipindi vinne kwa mwaka.Kalenda ya Ufugaji Nyuki Tanzania imegawanyika katika misimu minne kulingana na majira kwa mwaka ambayo hutofautiana kati ya mkoa na mkoa.
Katika kila msimu kazi za mfugaji Nyuki hutegemea kundi la Nyuki linahitaji nini na mfugaji afanye nini kuweza kuzalisha mazao ya Nyuki.

MSIMU WA NJAA KWA NYUKI
Ni kipindi cha kiangazi ,ukame na mimea mbalimbali imepukutisha maua na majani.
Matokeo.
·        Chakula kinakuwa kidogo kwenye mzinga
·        Idadi ya Nyuki hupungua mzingani
·        Malkia hupunguza au huacha kutaga mayai kabisa.
·        Makundi ya Nyuki kuhama kutafuta sehemu zenye malisho(ubichi)
·        Baadhi ya makundi ya Nyuki hupita kwenye kundi lenye asali kuiba.
Wajibu wa Mfugaji Nyuki katika msimu huu.
·        Chukua tahadhari ya mizinga usivamiwe na maadui wa nyuki mfano sisimizi,nyegere na wengine wanaotaka kuingia ndani ya mzinga.
·        Makundi yakingwe kutokana na jua kali na upepo.
·        Andaa vifaa vya ufugaji nyuki(kutengeneza mizinga,kukarabati iliyo mibovu)
·        Lisha makundi ya Nyuki imara kwa asali kama njaa ni kali.
MSIMU WA KUJIJENGA KWA NYUKI.
Hiki ni kipindi ambapo mvua za awali zimeanza na mimea inachanua kwa wingi.Makundi ya Nyuki hupita kutafuta makazi pia huzungukazunguka kwenye mzinga na sehemu nyingine.
Matokeo
·        Nyuki hujenga masega ya asali
·        Nyuki huzaliana kuongeza idadi yao kwenye mzinga
·        Makundi ya Nyuki hupita kutafuta makazi
·        Makundi huhama kwenye mizinga endapo kuna maadui au mzinga kuwa mbovu.
Wajibu wa Mfugaji Nyuki katika Msimu huu.
·        Fanya ukaguzi wa mizinga na manzuki kuwa katika hali ya usafi.
·        Safisha na kuambika mizinga isiyo na  Nyuki.
Tafuta makundi ya Nyuki ili kuwezesha mizinga kuwa na Nyuki kwa njia ya;
Ø Kutundika mizinga ya kukamatia makundi sehemu ambapo makundi ya Nyuki hupitapita.
Ø Kugawa makundi makubwa.
Ø Kuzalisha makundi ya Nyuki.
·        Saidia Nyuki kuongeza kiota kwa kuweka sanduku la ziada
·        Hakikisha Nyuki wana chakula cha kutosha
·        Kagua mizinga ya kisasa ya viunzi na vuna mzinga uliobebeshwa endapo una asali iliyokomaa
·        Tembelea mara kwa mara mizinga yenye makundi ya Nyuki kuona maendeleo au matatizo.
MSIMU WA MTIRIRIKO WA ASALI KWA NYUKI.
Ni kipindi ambapo miti na vichaka vimechanua maua kwa wingi na Nyuki wanatembelea maua kukusanya mbochi na chavua.Wakati huu ukipita karibu na mimea yenye maua utasikia sauti za Nyuki.
Matokeo.
·        Nyuki hukusanya mbochi na kuibadilisha kuwa asali.
·        Maadui wa Nyuki mfano siafu,sisimizi na wengineo huongezeka jirani na kundi la Nyuki.
·        Nyuki huongezeka kwenye kundi pamoja na kutengeneza masega.
·        Nyuki hupita kutafuta maji.
·        Weka kumbukumbu za maendeleo ya kila kundi na manzuki
·        Jenga ushirikiano na wafugaji Nyuki jirani kwa ajili ya kushughulikia changamoto zinazojitokeza kwa pamoja.
Wajibu wa Mfugaji Nyuki katika msimu huu.
Ø Fanya ukaguzi wa mara kwa mara kwenye manzuki na mizinga ya Nyuki.
Ø Fyeka majani na matawi ambayo yanasonga mizinga ya Nyuki.
Ø Wekea vizuia wadudu kupanda  kwenye mzinga wa Nyuki wa Nyuki hasa ile inayokaa kwenye vichanja
Ø Weka masanduku ya ziada kubebesha kwenye mizinga ya viunzi ili kuongeza uzalishaji,
Ø Fanya maandalizi ya vifaa vya kuvunia na kuhifadhia asali.
Ø Vuna baadhi ya masanduku yaliyobebeshwa endapo yana asali.
Ø Anza kutafuta masoko ya Asali unayokadiria kuvuna.
Ø Weka kumbukumbu za maendeleo ya kila kundi.
MSIMU WA MAVUNO KWA MFUGAJI NYUKI.
Ni kipindi ambapo maua ya mimea yamepungua na kuanza kutoa mbegu ama matunda,kiangazi ndio kinaanza.Sehemu nyingine baada ya kuisha mvua za vuli.Ni matunda ya kazi ya misimu mitatu iliyotajwa hapo juu na ni jukumu la Mfugaji wa Nyuki kuvuna mazao ambayo nyuki wamemuandalia.
Matokeo.
·        Nyuki huongeza ulinzi nje ya mzinga na huwa wakali
·        Baadhi ya mizinga nyuki hujikusanya nje.
·        Nyuki hupunguza kupitapita kwenye maua au kuhama.
Wajibu wa Mfugaji Nyuki katika Msimu huu.
·        Vuna masega yenye asali iliyokamaa.
·        Tumia bomba la moshi,mavazi ya kinga na vyombo safi wakati wa kuvuna.
·        Bakiza masega kiasi yenye asali kuwezesha Nyuki kutumia kama akiba.
·        Chuja asali na kuhifadhi katika eneo sahihi kulingana na ushauri wa kitaalamu.
·        Andaa nta endapo masega yametoka kwenye mizinga ya miche.
·        Tafuta masoko na kuuza mazao ya Nyuki.
·        Weka kumbukumbu za mavuno kwa kila mzinga na manzuki.
·        Toa taarifa zinazohusiana na mavuno na mauzo ya mazao ya Nyuki kwa Maafisa Ugani waliokaribu.

MABADILIKO YA KALENDA YA UFUGAJI NYUKI.
Sehemu ambazo zinapata mvua za vuli na masika kuna kuwa na msimu mdogo wa mavuno na msimu mkubwa wa mavuno.
Msimu mdogo wa mavuno huwa ni katika kipindi cha;
Mwezi Disemba/Januari(siku 14 tu) – Misitu ya miombo.
Mwezi February(Siku 14 tu) – Vichaka vya nang’ana.
ANGALIZO: EPUKA KUCHEMSHA ASALI.Asali iliyokamuliwa vyema na kuhifadhiwa vizuri mahali pasafi bila kuchemshwa huwa ASALI MBICHI ILIYO BORA.

Kwa maoni/Ushauri niandikie;
fabianbalele@gmail.com


Wednesday, February 17, 2016

HIVI NDIVYO KILIMO CHA MATUNDA KINAVYOWEZA KUKUTOA KIMASOMASO..

MIEMBE NA MIPARACHICHI.

Iwapo utatumia miche iliyoungwa/kubebeshwa(Grafted). Miembe  huzaa matunda  baada  ya miaka 2- 3 baada ya kupandwa shambani.Hali kadhalika kwa Maparachichi.Mwembe mmoja huweza kutoa kati ya Matunda 300-800 kwa mwaka,hii hutegemea aina ya mwembe,ukubwa wa mti,ukubwa wa matunda na kiwango cha utunzaji.

Matunda hukomaa baada ya siku 90 hadi 120 tangu kutunga.Mti mmoja wa Mparachichi huzaa matunda 200 hadi 1000 kutegemea umri wa mti,udongo na utunzaji wa shamba na miti yenyewe.

JINSI KITAKAVYOKULIPA.
Kwa hekta moja uliyopanda, ina uwezo wa kubeba miti kuanzia 500 hivi.Tuchukulie miti 500 kama wastani tu, tukichukuwa makadirio ya mti mmoja kwa wastani kuzaa matunda 500,hivyo hekta moja itakuwa na matunda 250,000.Kama utakuwa na hekta mbili tu inamana hapo unahesabu matunda yako 500,000.

Ukifanikiwa kuuza kwa bei ya jumla,tuchukulie Sh.200 kwa kila tunda,hapo utakuwa umejipatia jumla ya Sh.100,000,000.(Milioni 100).

Wakati huo kabla ya kuvuna maembe/Maparachichi,unaweza kuweka shambani kwao mazao ya muda mfupi kama vile matikiti maji,kunde,maharage au matango.

Kwa ushauri/Maoni niandikie 

fabianbalele@gmail.com/ 0768937884.

Exclusive to Fabian Balele..






Monday, December 28, 2015

Mambo 10 Usiyoyajua Kuhusu Maisha ya "Nyuki"


1)Nyuki Malkia ni mkubwa kuliko Nyuki wengine katika kundi la Nyuki.
2)Nyuki Malkia ni jike pekee katika kundi la Nyuki mwenye uwezo wa kimaumbile wa kutaga mayai ingawaje kwenye kundi la Nyuki kuna majike wengi.
3)Nyuki Malkia ndiye Nyuki pekee mwenye uwezo wa kuishi muda mrefu zaidi,miaka mitatu hadi sita.
4)Nyuki VIBARUA ni majike ambao maumbile yao hayana uwezo wa kutaga mayai wala kujamiiana.
5)Nyuki dume hutokana na mayai ya Malkia yasiyorutubishwa na mbegu za kiume na kuwafanya nyuki hao kuwa na mzazi mmoja pekee yaani mama.
6)Nyuki dume hawana mshale wa sumu kwa ajili ya kujilinda dhidi ya maadui,badala yake wana uume.
7)Dume mmoja huweza kujaniiana na Malkia Mara moja tu ktk maisha take.
8)Baada ya tendo la kujamiiana Nyuki Dume hufa SAA chache kutokana na uume wake kukatika wakati wa kujamiiana.
9)Kwa hali hii,hata Nyuki vibarua hawajawahi kuwaona baba zao.
10)Kuna takribani aina tofauti elfu ishirini (20,000) za Nyuki wanaouma Duniani.



©Exclusive to "Balele Mwanahabari"..


Kwa maoni/Ushauri
0768937884 
fabianbalele@gmail.com

SIFA ZA SHAMBA LA NYUKI (MANZUKI)


Kuwapo Kwa mimea inayotoa Maua yanayotoa chakula cha nyuki cha kutosha, Kwa mfano,sehemu yenye misitu, shamba la miti au mazao ya kilimo. Muda wa mimea kuchanua ujulikane kwa mfugaji nyuki ili aweze kupanga muda ambao atawezesha kundi la nyuki kujijenga na kukusanya mazao ya kutosha wakati mimea inapochanua Maua. 

Maji ya kutosha ni muhimu, nyuki huyatumia kupooza kupooza joto ndani ya mzinga, kulainisha chakula na kurekebisha utamu wa asali ambayo hulishwa majana. 

Mahali panapofikia ili kuwezesha usafirishaji wa vifaa na mazao ya nyuki nyakati za uvunaji. 

Umbali wa kilomita tatu kutoka katika makazi ya watu,shule,hospitali na pasiwe mahali ambapo ni mapito ya Mifugo. Inapolazimu kuwa na Manzuki katika maeneo haya ,izungushiwe uzio wenye miti mirefu ili nyuki wanapokwenda nakurudi kutafuta cha kula wapiti juu  ili wasishambulie watu na wanyama. Umbali uliotajwa hapa ni kwa ajili ya nyuki  wanaouma tu. 

Mbali na maeneo ya kilimo kinachotumia kemikali kwa mfano kilimo cha tumbaku na korosho, Manzuki yaanzishwe umbali wa kilometa saba kutoka maeneo hayo. Hii ni kuzuia nyuki wasife kwa kemikali hizo, au kuzuia mizinga isiangushwe na pia kusababisha nyuki washindwe kurudi kwenye mizinga.
Kudhibiti uharibifu kutokana na maadui wa nyuki, wizi wa mizinga na mazao ya nyuki.

Viashiria Vifuatavyo hutumika sehemu mbalimbali kutambua muda wa kuvuna Asali..
i)Mwisho wa Msimu wa mvua na mwanzo wa Kangazi

ii)Maua au matunda ya mmea Fulani kupukutika

iii)Matunda ya mmea mwitu kutokeza

iv) Mazao ya shamabani kukomaa

v)Mng’urumo wa nyuki wakusanyao chakula kupungua

vi)Madume ya nyuki kuonekana yamekufa kwenye mlango ama chini ya mzinga

vii)Kundi la Nyuki kutanda nje ya Mzinga

viii)Gundi nyingi kuonekana katika mlango na matundu ya Mzinga

ix) Uzito wa Mzinga kuongezeka

x)Kijiti kuchomwa ndani ya Mzinga na kuona kama kina asali(Ukaguzi wa kienyeji)Njia hii haimuwezeshi mfugaji kujua kama asali imeiva ama mbichi.

xi)Sauti ya mzinga unapogongwa,inaashiria kama mzinga umejaa ama ni mtupu.

xii)Mwinamo wa mzinga kubadilika.
Muda wa Uvunaji asali baada ya kundi kuingia kwenye mzinga hutegemea mambo yafuatayo;
i)Kiwango cha maua yanayopatikana kwenye eneo la shamba la nyuki.

ii)Muda ambao maua hayo yanapatikana.

iii)Hali ya Hewa ya eneo hilo

iv)Ukubwa wa Kundi

v)Uwezo wa Nyuki kukusanya Nekta



KWA MAONI/USHAURI  
0768937884
fabianbalele@gmail.com




 

AINA ZA NYUKI NA TABIA ZAO


Nyuki ni jamii ya wadudu wenye jozi mbili za mabawa mepesi yenye mishipa laini.Nyuki huishi maisha ya kijamaa.Mwili wa Nyuki umegawanyika katika sehemu kuu tatu;kichwa ,kifua na tumbo(fumbati).Tofauti na wadudu wengine,nyuki hutengeneza na kuhifadhi Asali kwenye masega.

Kuna takribani aina tofauti elfu ishirini(20,000) Duniani.Nyuki hawa wanatofautiana kwa maumbile,ukubwa na tabia,lakini wote wanashahabiana kwa tabia moja ya kutembelea maua ili kukusanya mbochi(maji matamu yanayotengeneza asali) na chavua(unga unaopatikana kwenye maua) kwa ajili ya chakula chao.

Kuna jamii kuu mbili za Nyuki wanaopatikana Tanzania;Nyuki wanaouma na wasiouma.

NYUKI WANAOUMA
Nyuki wanaouma wanaopatikana Tanzania wamegawanyika katika makundi matatu kutegemea mahali wanapoishi.Wapo nyuki wanaoishi;
Sehemu za Mwambao(Pwani) wana umbo dogo na niwakali(Apis mellifera litorea),sehemu kame na tambarare,wana umbo la wastani,wakali kiasi na hutoa asali kwa wingi(Apis mellifera scutellata),sehemu za milimani,(zaidi ya futi 6,000 kutoka usawa wa Bahari) wana umbo kubwa na wapole,jina la kitaalamu wanaitwa Apis mellifera monticola.

NYUKI WASIOUMA
Nyuki wasiouma wanapatikana nchi za tropiki tu kama ilivyo Tanzania.
Nyuki wasiouma wanaishi ndani ya matundu ya miti,chini ya matawi makubwa ya miti,kwenye vichuguu vya mchwa na hata chini ya mapaa ya nyumba,nyuki hawa hu toa asali kidogo kulinganisha na nyuki wanaouma,Nyuki wasiouma wanaweza kutoa hadi lita 5 za asali kwa mwaka kutegemea na ukubwa wa mzinga,aina ,wingi wa nyuki na uwepo wa chakula(maua) cha kutosha.Asali ya Nyuki wasiouma inaaminika kuwa na uwezo mkubwa wa kutibu maradhi mablimbali kuliko asali ya Nyuki wanaouma.


JINSIA YA NYUKI NA MAJUKUMU YAO.
Kama ilivyo kwa viumbe vyote,nyuki nao waa jinsia mbili,nyuki dume na Nyuki Jike.Jinsia hizo ndiyo msingi wa mgawanyo wa majukumu ya kazi katika kundi la Nyuki.
Kundi la Nyuki wanaouma,lina aina tatu za Nyuki ambao ni Nyuki vibarua,malkia na dume.

NYUKI JIKE.
Jinsia hii inamakundi mawili ya nyuki amabyo hutekeleza majukumu mawili tofauti.

 a)Nyuki Malkia
NYUKI MALKIA(QUEEN)
Ni nyuki jike ambaye hulelewa kwa kula chakula rasmi(maziwa ya Nyuki) na kupata matunzo maalumu kwa maisha yake yote(tangu hatua ya yai hadi uzee wake wote)Chakula hiki humwezesha kuishi kati ya miaka miwili hadi sita.
Nyuki malkia ni mkubwa kuliko nyuki wengine katika kundi la Nyuki,tumbo lake ni refu lenye rangi ya njano na dhahabu ghafi.
Nyuki Malikia,hutoa kemikali(Pheremones)mwilini mwake kutoa miongozo  kwa kundi la Nyuki.Mpangilioo wote na Mgawanyo wa kazi katika kundi la nyuki hutegemea maelekezo yake.Kundi la Nyuki lisilo na Malkia hukosa mwelekeo na huishi kwa kipindi kifupi.

b)Nyuki Vibarua
Nyuki vibarua ni majike ambao maumbile yao hayana uwezo wa kutaga mayai wala kujamiiana na nyuki madume.Kwa kawaida nyuki vibarua ambao hawatagi mayai,ni majike tasaambao hawana uwezo wa wa kutaga mayai.Aidha,hufikia kuishi hadi siku 36.Wanaweza kufikia idadi ya 60,000 au zaidi katika kundi moja.

c)Nyuki dume
Hutokana na mayai ya Malikia yasiyorutubishwa na mbegu za kiumena kuwafanya nyuki hao kuwa na mzazi mmoja tu yaani mama,Nyuki dume ni wakubwa kuliko vibarua lakini wadogo kuliko Malkia.Macho yao ni makubwa na miili yao ina rangi nyeusi,nyuki dume hawana mshale wa sumu kwa ajili ya kujilinda dhidi ya maadui,badala yake wana uume.
Kazi kubwa ya Nyuki dume ni kujamiiana na malkia.Dume mmoja huweza kujamiiana na malikia mara moja katika maisha yake.,Baada ya Tendo la kujamiiana Dume hufa saa chache kutokan na uume wake kukatika wakati wa kujamiiana.

Kwa hali hii hata Nyuki vibarua hawajawai kuwaona baba zao.!

Kazi ya pili ya Nyuki madume ni kurekebisha hali ya hewa ndani ya mzinga kwa kupasha joto kiota hasa wakati wa Usiku kwa kukumbatia juu ya kiota,sehemu ya watoto.Wakati wa upungufu mkubwa wa chakula au kiangazi nyuki madume hutolewa na vibarua nje ya mizinga na baadea hufa kwa njaa au baridi.

Kwa Maoni/Ushauri
0768937884
fabianbalele@gmail.com







Tuesday, September 30, 2014

MASWALI YANAYOULIZWA MARA KWA MARA KUHUSU UFUGAJI WA NYUKI





UFUGAJI WA NYUKI NI NINI?
Ufugaji wa Nyuki ni kuhifadhi nyuki ndani ya Mizinga kwa Madhumuni ya  kupata mazao ya nyuki kama vile asali,nta na gundi

NYUKI HUFUGWA WAPI?
Nyuki wanaweza kufugwa mahali popote penye mimea inayotoa maua ya kufaa.
MAMBO MUHIMU YA KUZINGATIA UNAPOCHAGUA SEHEMU YA KUFUGIA NYUKI.
1)Chunguza kama ipo Mimea ya Maua ya kufaa na kutosha,kwa mfano uoto wa asili kama vile miombo,au mashamba ya miti au mazao ya kilimo.
2) Chunguza Kama kuna maji ya kutosha naya kudumu.Endapo hakuna maji hakikisha unaweka maji kwa kuwajengea visima vidogo vidogo au hata kwenye madebe au makopo.
3) Chunguza kama pana athari za mafuriko ya mara kwa mara ili mizinga yako usizolewe na maji.
4) Chunguza kama sehemu uliyochagua inapitika nyakati zote za mwaka na ina kivuli cha kutosha 
5) Chunguza kama sehemu uliyochagua haina upepo mkali kupita kiasi. Upepo mkali unaozidi kilometa 80 kwa saa utazuia nyuki kutoka nje au kupotea kwa kusombwa na upepo.
6) Chunguza kama sehemu hiyo haina maadui wa mizinga  na nyuki kwa mfano nondo, nyegere, wezi, mchwa, siafu n.k.
7) Hakikishha sehemu utakayochagua iko mbali na barabra kuu au shughuli za jumuiya, mfano, soko, kanisa, msikiti, shule, makazi ya watu, hospitali n.k.
IDADI GANI YA MIZINGA IWEKWE KWENYE MANZUKI?
Idadi ya mizinga inayotakiwa kuwekwa kwenye manzuki inategememea wingi na aina ya mimea inayotoa maua katika  sehemu husika. Inashauriwa kutokuweka mizingi mingi kupita uwezo wa eneo la kufugia nyuki.
Makadirio ya idadi ya mizinga kwenye eneo la mita 120 za mraba katika uoto mbalimbali yameoneshwa kwenye jedwali namba 1
Jedwali Na 1: Idadi ya mizinga kwenye eneo la mita za mraba 120 kwa maeneo mbalimbali
NA
AINA ZA UOTO
IDADI YA MIZINGA
1
Miombo yenye miti mingi
5 - 10
2
Miombo yenye miti ya hapa na pale
5
3
Misitu minene
15 au zaidi
4
Misitu ya kupandwa yenye miti inayotoa maua
15 au zaidi
5
Shamba la katani
15 au zaidi
6
Shamba la Michungwa
15 au zaidi
7
Shamba la mazao ya kilimo mchanganyiko
5
8
Mkusanyiko wa uoto anuai kama vile vichaka na mbuga za majani.
2 - 4

JINSI YA KUTEGA MAKUNDI YA NYUKI ILI KUANZINSHA MANZUKI
1.    Mizinga mipya kabla ya kutundikwa ni budi iwekwe chambo. Chambo kinachotumika zaidi ni nta. Nta iliyoyeyushwa na kupakazwa ndani ya mzinga hutoa harufu ambayo huwavutia nyuki. Mizinga iliyowekwa chambo hutundikwa juu ya miti kwa kutumia waya kusubiri makundi ya nyuki yapite.
2.   Njia nyingine ni kugawa kundi kubwa la nyuki na kugawia kwenye mzinga mpya au usiokuwa na nyuki. Masenga mawili, moja lenye majana na mayai na moja lenye asali au chavua pamoja na nyuki wasiopungua 100 huhamishwa kwenye mzinga mpya. Mzinga uliogawiwa nyuki (mpya) unawekwa pale ambapo mzinga wa zamani ulipokuwa na wa zamani unahamishwa.
3.   Njia nyingine ni kukamata makundi ya nyuki yaliyojikusanya kwenye tawi la mti na kulikung’utia ndani ya boksi au mzinga mdogo halafu unakwenda kuwaweka kwenye mzinga wako mpya. Nyuki hawa itabidi walishwe siku za mwanzo kwa kutumia asali au shira ya sukari kwa vile  watakuwa hawana chakula.
MAMBO YA KUFANYA KWENYE SHAMBA LA NYUKI
Utunzaji ya nyuki /shamba la nyuki kunalenga kupata mazao bora na ya kutosha ya asali na nta, pia faida zitokanazo na uchavushaji wa nyuki kwa mazao mbalimbali ya kilimo.
Katika kuhudumia makundi yako ya nyuki unahitajika kuwa na kalenda ya mfuga Nyuki. Kalenda ya mfuga nyuki ni utaratibu wa shughuli zote mfugaji anazotakiwa kuzifanya katika kipindi cha mwaka. 
Kalenda ya mfugaji nyuki inatambulika mfugaji shughuli gani ya kufanya na ambayo haijafahamika katika misimu mbalimbali ya mwaka.
Aidha,  ukaguzi wa makundi na uvunaji wa asali hufanywa kulingana na kalenda  ya ufugaji nyuki.
Kalenda za ufugaji wa nyuki hazifanani kwa kila eneo  la nchi. Hii inatokana na majira ya mwaka ambayo nayo ni tofauti tofauti kufuatana na sehemu ya nchi.
Yafuatayo ni maelezo ya kalenda ya mfuga nyuki pamoja na shughuli zinazohitaka kufanywa;
     Msimu wa njaa
Hiki ni kipindi cha kiangazi ambacho maua kwa ajili ya mbochi na chavua yameadimika . Aidha, akiba ya asali na chavua kwa ajili ya nyuki ni kidogo.
  
      Shughuli za kufanya katika kipindi hiki ni zifuatazo
·        Kukagua makundi kuangalia maadui wa nyuki, mfano, siafu, nondo n.k.
·        Kuwalisha nyuki, kwa kutumia shira ya sukari , au asali kama ipo ikiwa nyuki hawana akiba yeyote iliyosalia. Angalizo:Hapa Tanzania hakuna mazoea ya kulisha nyuki  isipikua mkulima/mfugaji akiamua mwenyewe.

Jinsi kulisha nyuki
·        Tengeneza mchanganyiko wa sukari na maji . sehemu 1 kwa 1 yaani kikombe 1 sukari na maji kikombe 1.
·        Chemsha maji mpakaka yachemke kisha ondoa motoni na ongeza sukari huku ukikoroga mpaka iyeyuke. 
·        Acha mchanganyiko upoe
·        Jaza mchanganyiko kwenye chombo cha kulishia nyuki
·        Angalia baada ya  siku tatu ili ikibidi uwaongezee nyuki chakula

Msimu wa kujenga
Huu ni msimu wa nyuki wa kujenga, kwani kipindi hiki vichaka pamoja na miti michache inaanza kutoa maua na nyuki wanaanza kujenga masega ya kuweka asali tayari kwa msimu ujao  wa maua. Aidha , Malkia anataga mayai zaidi na nyuki wengi zaidi hutotolewa ili kuongeza nguvukazi kwente kundi la vubarua  kwani wengi watakuwa wamekufa kipindi cha njaa.
Shughuli za kufanya katika kipindi hiki ni zifuatazo
·        Kagua maadui wa nyuki katika mizinga
·        Unganisha makundi madogo ili kupata kundi kubwa
·        Kugawa baadhi ya makundi ikiwa ni makubwa ili yahamishiwe kwenye mizinga iliyohamwa. 
·        chunguza kama nyuki wanajenga masega vizuri kwehye vinzi au miche na siyo kwa kukatiza
·        usafi wa shamba

Msimu wa maua
Wakati huu vichaka vingi na mimea mingi inatoa maua,  nyuki wanakusanya chakula(mbochi na chavua ) kwa wingi pamoja na kuivisha asali.
Shughuli za kufanya katika kipindi hiki ni zifuatazo:
·        kupanua viota (kwa mizinga ya biashara), ina maana kuwa kama sanduku la chini limekaribia kujaa yaani liko robo tatu basi uongeze jingine la ziada juu yake baada ya kuweka kitenga malkia.
·        Kuangalia maadui.
·        Kuangalia kama asali imeshaiva na tayari kwa kuvuna
·        Kutafuta soko la kuuzia mazao yako(Asali,Nta,Gundi n.k)

Makala hii itaendelea tena………….
Imeandaliwa kwa Msaada wa kitabu cha  (R.P.C Temu,2007 ). Na msaada wa Mtandao/Internet.

Kwa Maoni /Ushauri: +255714759047/+255768937884

                        fabianbalele@gmail.com